Saturday 4 March 2017

Rais wa Chama cha Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo TCCIA, Ndibalema John Mayanja (katikati), akizungumza hii leo Jijini Mwanza kwenye mkutano na wadau mbalimbali wa biashara. Kulia ni Makamu Mwenyekiti TCCIA mkoani Mwanza, Leopord Lema, na kushoto ni Mshauri TCCIA mkoani Mwanza, Lazaro Kiheya.

BMGHabari
Rais wa Chemba ya Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo nchini TCCIA, Ndibalema Mayanja, amewahimiza watanzania kuchangamkia fursa ya ununuaji wa hisa za kampuni ya TCCI Investment.

Mayanja ameyasema hayo Jijini Mwanza hii leo na kubainisha kwamba hisa hizo zilianza kuuzwa tangu Februari Mosi mwaka huu kwa bei ya shilingi Mia Nne na kwamba mwisho wa uuzwaji wa hisa hizo ni Machi 14 mwaka huu.

"Njia pekee ya kijiendeleza kiuchumi hivi sasa ni kupitia hisa hivyo nunueni hisa hizi za kampuni ya uhakika ambayo kila mwaka huwapatia wanahisa wake gawiwo lao". Amesisitiza Mayanja na kuongeza kwamba hisa hizo zinauzwa katika benki ya CRDB na kwa mawakala mbalimbali walioidhinishwa na Mamlaka ya Masoko na Dhamana (CMSA).

Mwenyekiti wa TCCIA mkoani Mwanza, Joseph Kahungwa, amebainisha kwamba walionunua hisa za TCCIA Investment mwaka 2005 kwa shilingi 250, hisa zao zimepanda bei hadi shilingi 5,000 hivyo pesa hiyo iligawanywa na kupatikana bei ya shilingi 400 ya kuuza hisa mwaka huu ambapo kwenye mauzo hayo kila mwanahisa atapata gawio la hisa 12.5 kwa kila hisa moja.

Makamu Mwenyekiti TCCIA mkoani Mwanza, Leopord Lema, mesema jumla ya hisa Milioni 112 zinatarajiwa kuuzwa lengo ikiwa ni kampuni ya TCCIA Investment kupanua mtaji wake na kufikia Bilioni 45 kutoka Bilioni Nane za mwaka huu 2017 ambazo zimeongezeka kutoka hisa Bilioni Moja mwaka 2005 wakati kampuni hiyo inaanzishwa.

Amedokeza kwamba hatua hiyo itasaidia TCCIA kuongeza uwekezaji wake ikiwemo ujenzi wa majengo ya kisasa na maghara ya kuhifadhia mazao katika mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Mtwara na Tanga pamoja na kuanzisha taasisi ya mikopo.
Makamu Mwenyekiti TCCIA mkoani Mwanza, Leopord Lema, akisisitiza juu ya umuhimu wa watanzanua kununua hisa za Kampuni ya TCCIA Investment. Pia amesema TCCIA itaendelea kushirikiana na serikali katika kuondoa changamoto za kiuwekezaji zilizopo ikiwemo upimaji wa maeneo ya ujenzi wa viwanda pamoja na uwanja wa maonesho ikiwemo Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki
Mshauri TCCIA mkoani Mwanza, Lazaro Kiheya akitoa neno la shukurani kabla ya mkutano huo kuahilishwa. Kulia ni Rais wa TCCIA, Ndibalema Mayanja.
Meneja Elimu kwa Mlipa Kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA mkoani Mwanza, Lutufyo Mtafywa (kulia), akizungumza kwa niaba ya meneja wa TRA mkoani Mwanza katika mkutano huo. 

Ameelezea umuhimu wa kila mfanyabiashara kuwa namba ya utambulisho wa biashara (TIN Number) na kuwasihi kutoa ushirikiano kwenye zoezi la uhakiki wa namba hizo ambapo amesema baada ya kufanyika Jijini Dar es salaam, litaendeleo Jijini Mwanza na maeneo mengine pia.
Mmoja wa wafanyabiashara waliohudhuria mkutano huo akiwasilisha maoni na ushauri wake
Baadhi ya wafanyabiashara na wadau wa biashara na uwekezaji wakifuatilia mkutano huo
Baadhi ya wafanyabiashara na wadau wa biashara na uwekezaji wakifuatilia mkutano huo
Picha ya pamoja.