Monday 24 August 2009

HUKUMU YA MAHAKAMA KUU DHIDI YA KESI YA AKINA ZOMBE - Hii hapa
Akimchambua mshitakiwa wa kwanza Zombe, Jaji alisema mshitakiwa huyo wakati wa mauaji yanafanyika alikuwa ndiye Kamanda wa Polisi na Mkuu wa Upelelezi; hivyo alikuwa na jukumu la kujua wahalifu hao walikohifadhiwa baada ya kukamatwa.
Alisema hata baada ya kusikia mauaji yametokea, Zombe hakuonesha nia ya kwenda kuona ambako ilidaiwa kulikuwa na mapambano kati ya polisi na majambazi badala yake alienda Kituo cha Polisi kuulizia fedha. “Hapa ni wazi kuwa ni kweli alijua kilichokuwa kinaendelea, lakini hata hivyo upande wa mashitaka umeshindwa kuonesha namna mshitakiwa huyu alivyoshiriki kwenye mauaji hayo,” alisema Jaji Massati.
Alikataa baadhi ya ushahidi uliotolewa kuwa Zombe aliwafundisha wenzake cha kujitetea kwenye Tume ya Jaji Kipenka Mussa. Lakini pia alisema madai kuwa Zombe siku ya tukio alikuwa anawasiliana na Bageni hazikuwa za kweli.
Kwa upande wa Bageni, Jaji Massati alisema licha ya kuwepo ushahidi wa kuongoza msafara hadi kwenye msitu wa Pande, na kutajwa na washitakiwa wawili kuwa ndiye aliyeamuru Koplo Saad afyatue risasi, ushahidi huo haukuungwa mkono na shahidi mwingine hivyo hauwezi kukubaliwa na mahakama.
“Kwa hali hiyo ushahidi wa namna hii hauwezi kukubalika kisheria, ni lazima uungwe mkono na mashahidi wengine jambo ambalo upande wa mashitaka walishindwa kulitimiza; hivyo nasema hana hatia juu ya kesi ya mauaji,” alisema.
Akimwelezea Mrakibu Msaidizi wa Polisi Ahmed Makelle, Jaji Massati alisema ushahidi uliopo mahakamani unathibitisha kuwa alikuwepo wakati washitakiwa wanakamatwa na alishiriki kuchukua mfuko uliokuwa na fedha.
Alisema kwa Ofisa Mwandamizi wa Polisi kama Makelle, alikuwa na wajibu wa kuchukua kielelezo hicho na kukihifadhi, lakini akasema kuwepo kwake pale hakuwezi kumtia hatiani kuwa alishiriki kwenye mauaji.
“Kinachomuunganisha mshitakiwa na marehemu ni hili begi la fedha, zaidi ya hapo hakuna mahali upande wa mashitaka umetoa ushahidi wa kuhusika kwake kuwaua marehemu, hivyo na yeye hana hatia,” alisema.


Read more: HUKUMU YA MAHAKAMA KUU DHIDI YA KESI YA AKINA ZOMBE - Hii hapa