Saturday 29 June 2013



MAAJABU YA BONGO MAITI YA FUFULIWA

BINTI aitwaye Nuru Omari anayedaiwa kufariki dunia mwaka 2010 ameibuliwa hivi karibuni wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani na mganga akiwa hai kwenye banda kuukuu. 
Binti Nuru Omari aliyeibuliwa.
Tukio hilo limetokea kwenye Kijiji cha Kalole, Tarafa ya Kisiju, walayani humo.
Kwa mujibu wa baba wa binti huyo, Omari Salum, mwaka 2010 ndugu wa mkewe aitwaye Nyasenene aliyekuwa akiishi Charambe Mbagala, jijini Dar alifika nyumbani kwake na kuwaomba wampe mtoto wao kwa ajili ya kwenda kufanya kazi za ndani ‘hausigeli’.


Kijumba alimokuwa Nuru.
Baada ya binti huyo kufanya kazi kwa muda mfupi aliugua malaria, baba mtu akapewa taarifa  na kufika Dar kwa ajili ya kumuona mwanaye  aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar.
Mzee huyo amesema alikwenda Muhimbili na kufanikiwa kuzungumza machache na mwanaye huyo ambapo alikuwa akilalamikia maumivu ya tumbo.

Ndugu na majirani waliofika kumtazama Nuru.
Mzee huyo alisema ilibidi aondoke licha ya mwanaye kumtaka alale lakini kwa vile yeye ni mwanaume isingewezekana kulala hospitalini hapo.
“Kesho yake nilipewa taarifa kuwa mwanangu amefariki dunia usiku. Tulianza taratibu za mazishi na  kumzika kwenye Makaburi ya Kichangani, Mbagala, Dar kutokana na kukosa fedha za kuusafirisha mwili hadi Mkuranga,” alisema mzazi huyo
Mganga wa kienyeji aliyejulikana kwa jina la Said Ali Ngaora ‘Dr. Lamba’ anayeishi Mbagala Rangi Tatu, Dar  alifika katika kijiji hicho cha Kalole mwaka huu na kuwaambia wananchi kuwa kijijini hapo pana mtu anaonekana alikufa na kuzikwa lakini bado yupo hai na amewekwa sehemu na kutaja gharama za kumtoa ni shilingi milioni tatu.

Mganga aliyemuibua Nuru.
Akielezea tukio zima Dr. Lamba alisema wananchi walimruhusu akaanza kazi kwa kushirikiana na wataalamu wenzake.
Dr. Lamba na timu yake walifanikiwa kumuibua msichana huyo anayekadiriwa kuwa na miaka 12-15 kwenye mji ambao hakuna mtu anayeishi akiwa ndani ya banda la kuku huku kukiwa na chungu chenye damu, asali na udongo ambavyo vilikuwa ndivyo vyakula vyake akiwa na muonekano wa kutisha kwa kuwa na nywele ndefu na chafu na kucha zikiwa ndefu mithili ya jini.
Baada ya kumtoa alipelekwa katika uwanja wa mpira kijijini hapo na kuogeshwa pamoja na kukatwa kucha kisha akapelekwa katika nyumba aliyofikia mganga huyo, hata hivyo hakuweza kuongea vizuri.
Kwa mujibu wa mashuhuda ulimi wa Nuru ulikuwa mzito na mpaka sasa anazungumza kwa vitendo kama bubu huku chakula ambacho ameanza kula vikiwa ni ugali na kuku, uji na juisi ya embe.
Mbali na shilingi milioni tatu za kutoa, mganga huyo anataka milioni 15  kutokana na  dawa anazompa  kwa ajili ya matibabu ili arudi katika hali ya kibinadamu .
Hata hivyo, baadhi ya ndugu wanaopinga kuwa Nuru siyo mtoto wao lakini baba mzazi anasema ni  mwanaye kutokana na alama zilizopo mgongoni mwake na  anafanana sana na mdogo wake.
Makamu Mwenyekiti wa kijiji hicho, Ali Hassan Ndeko alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema mpaka sasa  wanakijiji wanaendelea kumiminika kwa ajili ya kumuona mtoto huyo akiwa chini ya uangalizi maalumu wa mganga huyo huku wakijitolea vyakula.