Saturday 12 December 2015

MATUKIO MBALIMBALI YA MAADHIMISHO YA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA
Dar es salaam, Madereva wa boda boda wakiongoza maandamano ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake jijini Dar es salaam. Maandamano hayo yalianzia uwanja wa Tipi ulioko Sinza hadi katika hotel ya Blue Pearl iliyopo Ubungo.

Dar es salaam, Ujumbe mbalimbali wa maadhimisho ya kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.

Kilimanjaro, Maandamano yakipita eneo la kituo kuu cha Mabasi cha mjini Moshi yakieekea katika viwanja vya kituo hicho ambako uzinduzi wa kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kanda ya kaskazini
Kilimanjaro, Mkuu wa wilaya ya Moshi, Novatus Makunga akisikiliza malezo kutoka katika banda la shirika la NAFGEM linalopambana na vitendo vya Ukatili dhidi ya Wanawake.

Mwanza, Shirika la kutetea haki za wanawake la KIVULINI la jijini Mwanza likikabidhi zawadi mbalimbali zikiwemo laptop kwa waandishi walioandika habari zinazotetea haki za wanawake.


Kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia inahitimishwa leo tarehe 10 Disemba ambayo ni siku ya kimataifa ya tamko la Haki za Binadamu ikiwa ni ishara ya kuhusisha ukatili dhidi ya wanawake na haki za binadamu na kutia msisitizo kwamba ukatili kama huu ni ukiukwaji wa haki za binadamu.

Maadhimisho haya yalianza rasmi tarehe 25 Novemba siku ambayo ilichaguliwa na Umoja wa Mataifa mwaka 1993 kuwa ni siku ya kimataifa ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake ambapo kila mwaka, Umoja wa Mataifa unashauri, mashirika ya Kimataifa na asasi zisizo za kiserikali kufanya shughuli zinazolenga kufahamisha jamii juu ya ukatili wa kijinsia, hususani ukatili dhidi ya wanawake.

Mwaka huu, kauli mbiu inasema FUNGUKA, CHUKUA HATUA, MLINDE MTOTO APATE ELIMU yenye lengo la kuhamasisha jamii kutambua changamoto mbalimbali zinazohatarisha usalama na kuchochea ukatili wa kijinsia mashuleni ikiwa ni pamoja na suala la viboko kuendelea kuwa tatizo kubwa, adhabu kali wanazopewa watoto ambao haiendani na umri wao pamoja na mila na desturi potofu zinazokandamiza watoto wa kike kama mimba za utotoni na ukeketaji.

Video: Uzinduzi wa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia: https://www.youtube.com/watch?v=TdGTQiAi4Fg

Mkurugenzi wa shirika la WiLDAF, Dr. Judith Odunga akizungumza wakati wa ufunguzi wa kampeni hizi alitaja changamoto nyingine kuwa ni miundombinu ambayo ni pamoja na kuwa na madarasa ya kutosha, madawati, vyoo na sehemu za kujisitiri kwa watoto wa kike, mabweni, uzio kuzunguka mashule pamoja na mazingira magumu ya usafiri wakati wa kwenda na kurudi nyumbani na kutokuwa na chombo cha wanafunzi cha kutumika kusemea matatizo yao pale ambapo wanakutana na changamoto mbalimbali.

Akiongezea, Dr. Odunga alisema kampeni hii kwa mwaka huu ilifanyika kikanda chini ya uratibu wa mashirika na wadau mbalimbali wa maendeleo. Kanda hizo ni kanda ya Ziwa (Mwanza, Mara na Shinyanga), Kanda ya Kaskazini (Manyara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga), Kanda ya Kati (Dodoma, Morogoro na Singida), Kanda ya Kusini (Mtwara, Songea, Mbeya, Iringa na Lindi), Kanda ya Pwani (Dar es salaam na Pwani) na kuratibiwa na wadau mbalimbali wakiwemo mashirika ya KIVULINI, CWCA, NAFGEM, Morogoro Paralegal,  Mtwara paralegal, WiLDAF, TWCWC pamoja na Jeshi la Polisi.

Ujumbe wa maadhimisho haya na picha zinapatikana kupitia ukurasa wa Facebook wa WILDAF ambao ni www.facebook.com/WILDAFTZ