Monday 14 July 2014

“Ni kweli nilishiriki kwenye maziko kwa sababu mimi kama Balozi wa Tanzania wakati huo ndiye nilikuwa mwakilishi wa Serikali pale Washington, lakini jambo la pili ni kwamba binafsi nilimfahamu Ballali kwa muda mrefu, kwa hiyo hata kama nisingekuwa balozi lazima ningekwenda kuzika tu.” Balozi Ombeni Sefue.
---
  Gavana wa zamani wa Benki Kuu ya Tanzania BOT), Marehemu Daudi Ballali aliacha wasia unaotaka maiti yake isionyeshwe hadharani atakapofariki dunia na wala maiti yake isiletwe Tanzania kwa ajili ya maziko.

Ballali aliyefariki Mei 16, 2008 na kuzikwa Mei 23 mwaka huohuo katika makaburi ya Gate of Heaven, eneo la Silver Spring, Maryland nchini Marekani alifahamu kuhusu kifo chake wiki mbili kabla, baada ya matibabu kushindikana.
 
Mwandishi wa Mwananchi aliyekuwa nchini Marekani kwa siku kumi kufuatilia suala hilo, alibaini kuwa kiongozi huyo alilazwa mara ya pili katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha George Washington, April 2008 na alirejea nyumbani kwake, Washington DC wiki mbili kabla ya kukutwa na mauti.
 
Habari kutoka ndani ya familia yake zinasema baada ya madaktari kushindwa kumtibu walimwambia kwamba asingeweza kuishi kwa zaidi ya wiki mbili, hivyo walimshauri ahamie kwenye ‘hospice’ ambayo ni nyumba maalumu ya kusubiri kifo kwa watu ambao magonjwa yao yameshindikana.
 
Hospice hutumika kwa ajili ya kuwaweka wagonjwa wanaohitaji faraja hasa kutoka na maumivu makali chini ya uangalizi wa washauri na wauguzi kwa lengo la kuwaongezea wagonjwa husika siku za kuishi.

 Baadhi ya hospice hutoa huduma za kiroho, kijamii na kifedha na wakati mwingine huduma hizo hutolewa kwa wagonjwa ambao wanaugulia nyumbani. Hata hivyo, gazeti hili lilidokezwa kwamba Ballali alikataa kwenda kwenye nyumba hiyo na badala yake kutaka apelekwe nyumbani kwake.

 
“Alikataa kwenda kwenye hospice, aliwaambia madaktari kwamba yeye hawezi kwenda huko ijapokuwa kuna huduma nzuri na uangalizi wa nesi (muuguzi). Aliwaambia kwamba nitakwenda kufia nyumbani kwangu maana nina nyumbani kwangu,” kilisema chanzo chetu na kuongeza:

 “Aliporejeshwa nyumbani, alikuwa anazungumza kama kawaida lakini kadri siku zilivyosogea hali ilikuwa ikibadilika na kama sikosei siku mbili au tatu za mwisho (za uhai wake) alikuwa anajitambua lakini alikata kauli, hakuwa akizungumza chochote”.

 
Uchunguzi wetu umebaini kuwa katika siku hizo za mwisho za uhai wake, Ballali aliacha maelekezo kwamba pindi atakapofariki dunia, mwili wake usiwekwe hadharani kwa maana ya kutazamwa na watu nje ya familia wala kusafirishwa kuja Tanzania kwa ajili ya maziko.

“He said, he doesn’t like to be turned into a laughing staff (alisema asingependa kugeuzwa kichekesho), sababu watu wasingekuja kutoa heshima za mwisho, bali wangekuja kumdhihaki kuangalia Ballali aliyetuhumiwa kwa ufisadi wa EPA na siyo Gavana,” kilisema chanzo hicho.